Sunday, March 4, 2018

UN YASIMAMISH SHUGHULI ZAKE NIGERIA BAADA YA WAHUDUMU WAKE KUUAWA

UN yasimamisha shughuli zake Nigeria baada ya wahudumu wake kuuawa
Umoja wa Mataifa umetangaza habari ya kusitisha shughuli zake za utoaji huduma na misaada ya kibinadamu kaskazini mashariki mwa Nigeria kutokana na kuuawa wafanyakazi wake katika mashambulizi ya hivi karibuni ya magaidi wa Boko Haram.
Taarifa ya Msemaji wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa imesema kuwa, wahudumu 40 wa UN walikuwa katika mji wa Rann ambao una kambi ya wakimbizi wa ndani wapatao 55 elfu ulipovamiwa Alkhamisi usiku na wapiganaji wa Boko Haram.
Amesema kufuatia hujuma hiyo, Umoja wa Mataifa umesimamisha kwa muda utoaji wa huduma za kibinadamu katika mji huo ulioko kaskazini mashariki mwa Nigeria.
Wapiganaji wa kundi la kigaidi la Boko Haram
Siku ya Ijumaa, shirika la madaktari wasio na mipaka lilitangaza habari ya kusimamisha shughuli zake zote kaskazini mwa Nigeria baada ya genge la wakufurishaji la Boko Haram kuushambulia mji wa Rann katika jimbo la Borno, kaskazini mashariki mwa Nigeria.
Katika shambulizi lililofanywa na genge hilo Alkhamisi usiku, watu 11 wakiwemo wafanyakazi watatu wa kutoa misaada waliuawa huku wengine watatu wakihofiwa kutekwa nyara baada ya hujuma hiyo.
Mashambulizi ya magaidi wa Boko Haram nchini Nigeria na katika nchi jirani za Chad, Niger, na Cameroon yameshapelekea zaidi ya watu 20 elfu kuuawa na milioni mbili na laki sita wengine kuwa wakimbizi.

No comments:

Post a Comment