Friday, March 30, 2018

UTAFITI: WAKONGOMANI 8 KATI YA 10 HAWAMUUNGI MKONO RAIS KABILA WA DRC

Utafiti: Wakongomani 8 kati ya 10 hawamuungi mkono Rais Kabila wa DRC
Utafiti mpya wa maoni umeonyesha kuwa, kwa kila raia kumi wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, wanane hawamungi mkono Rais Joseph Kabila wa nchi hiyo.
Utafiti huo uliofanywa mwezi jana na shirika la utafiti la Congo Research Group CRG likishirikiana na Kituo cha Utafiri wa Maoni cha BERCI katika Chuo Kikuu cha New York unaonyesha wazi kuwa, akthari ya Wakongomani wamechoshwa na uongozi wa miaka 17 wa Rais Kabila na wangetaka kumuona akiachia ngazi.
Joseph Kabila alikataa kuachia madaraka baada ya kumalizika muhula wake wa utawala kikatiba mwaka 2016, na mpaka sasa hajajitokeza hadharani kusema iwapo ataachia ngazi baada ya uchaguzi wa rais unaotazamiwa kufanyika Disemba 23 mwaka huu au la.
Moise Katumbi, mwanasiasa mjasiriamali wa DRC
Kwa mujibu wa utafiti huo wa maoni uliowashirikisha Wakongamani elfu moja katika mikoa yote 26 ya nchi hiyo, asilimia 95 ya waliohojiwa wanasema wako tayari kushiriki uchaguzi rais wa mwezi Disemba; ambapo asilimia 26 wanasema wangelimchagua Moise Katumbi, kiongozi wa upinzani aliyeko uhamishoni, huku asilimia 13 wakisema wangelimchagua mwanasiasa mwingine wa upinzani Felix Tshisekedi kurithi mikoba ya Kabila.
Utafiti mwingine wa maoni uliofanywa mwaka mmoja uliopita na CRG na BERCI ulionyesha kuwa, asilimia 38 ya wapiga kura nchini humo wako tayari kumpigia kura Katumbi, na yumkini kiwango hicho kimeshuka ikilinganishwa na utafiti wa mwaka huu, kutokana na mwanasiasa huyo tajiri kutokuweko nchini kwa miaka miwili sasa

No comments:

Post a Comment