Friday, March 30, 2018

TUNDU LISSU : KINACHOWAPATA VIONGOZI WA UPINZANI TANZANIA, NI NJIA YA KUELEKEA IKULU

  
Tundu Lissu: Kinachowapata viongozi wa upinzani Tanzania, ni njia ya kuelekea Ikulu       
Mbunge wa Singida Mashariki na Rais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) nchini Tanzania, Tundu Lissu amesema kuwa, kile kinachowapata viongozi wa chama kikuu cha upinzani cha Demokrasia na Maendelea (CHADEMA), ni maandalizi ya upinzani huo kuingia madarakani.
Tundu Lissu ameyasema hayo ikiwa ni baada ya viongozi sita wa chama hicho ambao ni Mwenyekiti Taifa wa chama Freeman Mbowe, Katibu Mkuu Vincent Mashinji, Manaibu Katibu Mkuu, John Mnyika (Bara) na Salum Mwalimu (Zanzibar), Mweka Hazina wa Baraza la Wanawake Chadema (Bawacha), Esther Matiko na mbunge wa Iringa Mjini, Mchungaji Peter Msigwa, kushtakiwa kwa makosa manane na kisha kunyimwa dhamana.
Viongozi wa Chadema wakiwa kwenye gari la polisi baada ya kutiwa mbaroni
Kadhalika Lissu ambaye kwa sasa yuko nchini Ubelgiji kwa ajili ya matibabu, amefafanua kuwa, kilichowapata viongozi hao wa upinzani nchini Tanzania hakiwezi kuzima taa ya madai kwa ajili ya demokrasia ya kweli nchini humo. Viongozi hao wa chama cha Demokrasia na Maendelea (CHADEMA), walipelekwa jela siku ya Jumanne baada ya kupandishwa kizimbani na kusomewa mashtaka manane yakiwamo ya kufanya maandamano yaliyosababisha kifo cha Mwanafunzi wa Chuo cha NIT, Akwilina Akwiline, uasi, kuhamasisha chuki kati ya wanajamii na kuchochea ghasia nchini Tanzania.
Rais John Pombe Magufuli wa Tanzania
Hayo yanajiri katika hali ambayo siku chache zilizopita, Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe aliviambia vyombo vya habari kwa kuzituhumu asasi za serikali ya Dar es Salaam ikiwemo polisi kwamba, zilikuwa zinapanga mkakati wa kuwafungulia kesi ya mauaji na uhaini baadhi ya viongozi wa chama chake. Kwa mujibu wa Mbowe, lengo la kutekelezwa mkakati huo ni kuhakikisha kuwa viongozi hao wanawekwa mahabusu kwa muda mrefu ili kufifisha na kuua kabisa upinzani nchini.

No comments:

Post a Comment