Thursday, March 22, 2018

SALAMU ZA PONGEZI ZA TRUMP KWA PUTIN HASIRA ZA WAPINZANI WA RUSSIA NDANI YA UTAWALA WA MAREKANI

Salamu za pongezi za Trump kwa Putin na hasira za wapinzani wa Russia ndani ya utawala wa Marekani
Salamu za pongezi alizotoa rais wa Marekani kwa rais wa Russia kwa ushindi aliopata wa kuchaguliwa tena kuwa rais wa nchi hiyo katika uchaguzi uliofanyika hivi karibuni zimewakasirisha baadhi ya maseneta nchini Marekani.
Seneta wa chama cha Republican John MacCain amemtuhumu Rais Vladmir Putin wa Russia kuwa ni dikteta na kusema kwamba: kwa kumpa salamu za pongezi Vladmir Putin,Trump amewatusi wananchi wote wa Russia ambao wamenyimwa haki ya kupiga kura katika uchaguzi huru na wa haki ili kuamua kuhusu mustakabali wa nchi yao, ikiwemo idadi kubwa ya wazalendo wa Russia; watu ambao wamehimili hatari nyingi ili kuweza kutumia haki yao ya kulalamika na kupambana na utawala wa Putin.
Seneta John McCain (kulia) na Rais Vladmir Putin wa Russia
Madai hayo yanatolewa katika hali ambayo katika uchaguzi wa rais wa Russia uliofanyika hivi karibuni vyama na mirengo tofauti ya kisiasa ikiwemo ya wapinzani wakubwa wa Kremlin ilishiriki kwenye uchaguzi huo kuchuana na rais Putin. Hata hivyo kiongozi huyo ameweza kuvutia kura na mapenzi ya aghalabu ya Warussia kutokana na utendajikazi wake wa miaka 17 hususan mafanikio aliyopata ya kuitatua migogoro ya kisiasa, kiuchumi na kiusalama iliyotokana na kuvunjika Shirikisho la Kisovieti la Urusi ya zamani na kufufua tena nguvu na satua ya nchi hiyo katika uga wa kimataifa. Hali hiyo imetafsiriwa na kuelezewa na mirengo inayoipinga Russia katika nchi za Magharibi na hasa Marekani kuwa ni udikteta na hila za kutaka kuyatia mkono matokeo ya uchaguzi wa rais wa Russia uliofanyika hivi karibuni. Mrengo huo unaitumia kila fursa ikiwemo ya utoaji salamu za pongezi rais wa Marekani kwa rais wa Russia ili kuvuruga uhusiano wa Washington na Moscow, ilhali kuwasiliana kwa njia ya simu marais wa nchi mbili na kupongezana kwa kushinda katika uchaguzi ni jambo la kawaida na lililozoeleka. Takribani mwaka mmoja na nusu uliopita Putin alimtumia salamu za pongezi Trump aliposhinda uchaguzi wa rais wa Marekani uliofanyika mwaka 2016; na hivi sasa baada ya kupita siku mbili tangu kufanyika uchaguzi wa rais wa Russia, Trump naye amefanya vivyo hivyo kupitia mazungumzo aliyofanya kwa njia ya simu na Vladmir Putin. Lakini yeye amekwenda hata mbali zaidi kwa kueleza matumaini aliyonayo ya kupatikana fursa haraka iwezekanavyo ya kukutana na kufanya mazungumzo na rais wa Russia.
Trump (kulia) na Putin wameshakutana zaidi ya mara moja kwa mazungumzo
Mrengo unaoipinga Russia nchini Marekani una hofu baada ya kuona kwamba, licha ya propaganda kali za kueneza sumu dhidi ya Kremlin kwa kutumia visingizio mbalimbali kama kuingilia Russia uchaguzi wa rais wa Marekani sambamba na tuhuma mpya dhidi ya Moscow za kumpa sumu jasusi wa pande mbili wa Uingereza, Trump angali anafanya kila njia ili kuona uhusiano wa nchi yake na Russia unaboreka.
Tangu wakati wa kampeni za uchaguzi wa rais mwaka 2016 hadi sasa, rais wa sasa wa Marekani amesisitiza mara kadhaa kwamba bila ya kushirikiana na Russia baadhi ya mizozo mikubwa ya kimataifa hususan mgogoro wa vita vya Syria hautoweza kutatuka. Ni kwa sababu hiyo Trump angali anashikilia msimamo wake wa kuendelea kuwa na mawasiliano binafsi na rais wa Russia, kitendo ambacho kwa mtazamo wa baadhi ya watu kama John McCain, mkuu wa kamati ya huduma za vikosi vya ulinzi vya Marekani katika Seneti ya nchi hiyo, ni dhambi isiyosameheka.

No comments:

Post a Comment