Friday, February 2, 2018

AYATULLAH KHATAMI: LENGO KUU LA MAREKANI NI KUONDOA MFUMO WA KIISLAMU NCHINI IRAN

Ayatullah Khatami: Lengo kuu la Marekani ni kuondoa mfumo wa Kiislamu nchini Iran
Hatibu wa Swala ya Ijumaa ya leo mjini Tehran amesema kuwa, lengo na shabaha kuu ya Marekani ni kuupindua mfumo wa Kiislamu nchini Iran kupitia njama za kuushambulia mhimili wa Utawala wa Fakihi (Wilayatul Faqih) humu nchini.
Ayatullah Ahmad Khatami ameyasema hayo leo katika hotuba za Swala ya Ijumaa ya mjini Tehran na kuongeza kwamba, Marekani inafanya njama za kila namna za kutoa pigo dhidi ya nafasi ya juu ya Utawala wa Fakihi ambayo uongozi wake umepelekea kusambaratishwa njama mbalimbali za Marekani hasa katika kueneza makundi ya kigaidi likiwemo lile la Daesh (ISIS) katika eneo hili na kadhalika kusambaratisha njama za kuanzishwa Mashariki ya Kati Mpya kwa maslahi ya Marekani na Israel, na kwamba kusambaratishwa njama hizo kumeharibu ndoto kubwa ya Washington.
Saudia na utawala haramu wa Israel ambao ni watekelezaji wa njama za Marekani dhidi ya Iran
Akizungumzia stratijia mpya ya Marekani dhidi ya Iran ya Kiislamu amesema, stratijia hiyo inajumuisha kusambaratisha nishati ya nyuklia, kupunguza uwezo wa kiulinzi na uwezo wa makombora, kukata uungaji mkono wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kwa Harakati ya Kiislamu ya Hizbullah ya Lebanon na kwa wanamuqawama wa Palestina na kadhalika kuzuia upinzani wa Tehran wa kupambana na njama ya kuanzisha Mashariki ya Kati Mpya. Ayatullah Ahmad Khatami amesisitiza kwamba, viongozi wote wa mfumo wa Kiislamu nchini Iran wanapinga vikali hatua yoyote ya kufanya mazungumzo mapya ya nyuklia au kufanyiwa marekebisho mapatano ya nyuklia ya JCPOA na kupunguzwa uwezo wa kiulinzi wa makombora ya Iran ya Kiislamu na kwamba katika uwanja huo taifa hili halitoruhusu uingiliaji wowote wa kigeni nchini. 
Donald Trump, Rais wa Marekani ambaye njama zake na washirika wake dhidi ya Iran zimefeli
Hatibu wa Swala ya Ijumaa ya leo mjini Tehran ameashiria kwamba Jamhuri ya Kiislamu ya Iran inaendeshwa kwa mujibu wa sheria za Qur'an na katiba iliyosimama juu ya msingi wa mafundisho ya Kiislamu hivyo, itaendelea kuyaunga mkono makundi ya muqawama ya Palestina na harakati ya Hizbullah ya nchini Lebanon. Amefafanua zaidi kwa kusema, stratijia ya Washington katika eneo ni kuzusha machafuko kwa ajili ya kudhamini usalama wa utawala khabithi wa Kizayuni na kwamba, hivi sasa Marekani inalihamisha kundi la ukufurishaji la Daesh na kulipeleka Afghanistan kwa ajili ya kudhamini malengo yake ya kiuchumi na kisiasa katika eneo hili. Pia ameashiria jinai za hivi karibuni za utawala wa kidikteta wa Saudia nchini Yemen na matukio ya nchini Bahrain na kusema kuwa, hivi sasa Mohammad Bin Salman, Mrithi wa Kiti cha Ufalme nchini Saudia ameigeuza nchi hiyo kuwa kama moja ya majimbo ya Marekani.

No comments:

Post a Comment