Saturday, February 24, 2018

TAATHIRA ZA MAAMUZI HATARI YA TRUMP KUHUSU QUDS

Taathira za maamuzi hatari ya Trump kuhusu Quds
Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Palestina (Hamas) imelaani uamuzi wa Marekani wa kuhamisha ubalozi wake kutoka Tel Aviv na kuupeleka katika mji wa Quds unaokaliwa kwa mabavu.
Msemaji wa Hamas, Abdullatif al Qanou amesema kuwa hatua ya kuuhamisha ubalozi wa Marekani kutoka Tel Avid hadi Quds inayokaliwa kwa mabavu haiupatii utawala wa Kizayuni uhalali wowote  na wala haiwezi kubadili ukweli  wa mambo kuhusu mji wa Quds. 
Abdullatif al Qanou, Msemaji wa Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Palestina Hamas 
Msemaji Wizara ya Mashauri ya Kigeni ya Marekani, Heather Nauert amesisitiza kupitia taarifa iliyotolewa na wizara hiyo kwamba ubalozi mpya wa nchi yake huko Palestina inayokaliwa kwa mabavu utafunguliwa tarehe 14 Mei mwaka huu katika mji wa Quds (Jerusalem). 
Rais Donald Trump wa Marekani tarehe sita mwezi Disemba mwaka 2017 alitangaza kuwa, Washington imeutambua mji wa Baitul Muqaddas kuwa mji mkuu wa utawala wa Kizayuni wa Israel licha ya suala hilo kupingwa pakubwa kieneo na kimataifa na akasema Washington imeanza mchakato wa kutekeleza uamuzi huo. 
Mji wa Quds ambako kuna Msikiti wa al Aqsa ambao ni kibla cha kwanza cha Waislamu, ni eneo lisiloweza kutenganishwa na Palestina na ni miongoni mwa maeneo matatu matakatifu muhimu zaidi kwa Kiislamu. Kwa msingi huo uamuzi wa kifedhuli na kinyume cha sheria wa Rais wa Marekani wa kuhamishia ubalozi wa nchi hiyo huko Baitul  Muqaddas ni sehemu ya njama kubwa za Wazayuni na viongozi wa Marekani dhidi ya ulimwengu wa Kiislamu.   
Msikiti wa al Aqsa 
 
Chanzo na sababu za uamuzi huo uliodhidi ya Palestina na dhidi ya Uislamu wa Trump zinapaswa kutathminiwa katika mitazamo na itikadi zake kama mfuasi au muungaji mkoni wa Wakristo wa Kizayuni. Tangu aingine madarakani, Trump amekuwa akichukua hatua na maamuzi ya kichochezi na vitisho kuhusiana migogoro ya kimataifa na ya kikanda ikiwemo migogoro inayojiri katika eneo la Mashariki ya Kati; na mgogoro wa Palestina umefanywa ajenda kuu katika kalibu ya siasa na njama zinazofanywa na Marekani. Siasa hizo za kichochezi za Trump zinaweza kutathminiwa katika kalibu ya siasa jumla za White House katika eneo la Mashariki ya Kati katika fremu ya kile kinachojulikana kama "makubaliano ya karne." Fikra za waliowengi na duru za kisiasa katika eneo la Mashariki ya Kati zinayataja makubaliano hayo ya karne kuwa ni sehemu ya mipango yenye lengo la kuifuta kadhia nzima ya Palestina. Ni katika fremu ya mpango huo mpya wa Marekani kuhusiana na Quds utakaoishirikisha Israel ambapo Rais Donald Trump wa Marekani tarehe sita mwezi Disemba mwaka jana alitangaza  kuwa anautambua mji wa Baitul Muqaddas kuwa mji mkuu wa utawala bandia wa Israel.  
Rais Donald Trump wa Marekani  
Vilevile wachambuzi wa mambo wanasisitiza kuwa, lengo kuu la hatua ya Trump ya kuutambua utawala wa Kizayuni kuwa dola la Kiyahudi ni kuandaa mazingira ya kuwafukuza Wapalestina katika ardhi zao na kupinga suala la kuunda nchi ya Palestina mji mkuu wake ukiwa ni Quds na kukanyaga kikamilifu haki za Wapalestina. Katika mazingira kama hayo, Trump anafanya kila awezalo ili kuifuta kabisa kadhia ya Quds kwa kusaidiwa na kuungwa mkono na baadhi ya tawala za Kiarabu katika eneo hili. 
Gazeti la al Hayat linalochapishwa London limeandika kuwa: Israel inataka kunufaika na uamuzi wa Marekani wa kuhamishia ubalozi wake katika mji wa Quds ili kutekeleza njama ya kuufanya mji huo kuwa wa Kiyahudi. Gazeti hilo limenukuu mwandishi wa Kipalestina Nabil al Sahli akisema kwamba: Hatua za kuuhamishia ubalozi wa Marekani huko Quds inatekelezwa kwa kasi kubwa, suala linalodhihirisha taswira hatari ya maamuzi ya Rais Donald Trump wa Marekani dhidi ya Quds.
Naye Robin Wright mwandishi habari wa Kimarekani ameandika katika gazeti la New York kuwa: Hatua ya Donald Trump ya kuhamisha ubalozi wa Marekani kutoka Tel Aviv kwenda Quds itazidisha mgogoro katika Mashariki ya Kati.   
Hatua zote hizo za Trump hazitakuwa na natija nyingine ghairi ya kuimarisha Intifadha ya Tatu ya Wapalestina ambayo ilianza kujibu maamuzi ya Trump kuhusu Quds. Kwa kuzingatia hisia walizonazo Wapalestina na Ulimwengu wa Kiislamu na fikra za waliowengi duniani kwa ujumla kuhusu suala la Quds, hatua yoyote ile ya Marekani ya kuunga mkono na kuzibariki siasa za kiistikbari za Israel kuhusiana na Baitul Muqaddas inaweza kuigharimu Marekani kisiasa, kidiplomasia na kiuchumi. 

No comments:

Post a Comment