Saturday, February 10, 2018

WARUNDI WAANDAMANA BUJUMBURA KUPINGA RIPOTI YA UMOJA WA MATAIFA DHIDI YA NCHI YAO

Warundi waandamana Bujumbura kupinga ripoti ya Umoja wa Mataifa dhidi ya nchi yao
Maelfu ya raia wa Burundi Jumamosi ya jana waliandama mjini Bujumbura, katika kulalamikia ripoti ya hivi karibuni ya Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa inayopinga suala la kufanyiwa marekebisho katiba ya nchi hiyo ili kumruhusu Rais Pierre Nkurunziza kugombea katika uchaguzi ujao.
Katika maandamano hayo, Warundi walibeba mabango yaliyokuwa na jumbe za kumtuhumu Michel Kafando, mjumbe maalumu wa Umoja wa Mataifa nchini humo kwamba anatumikia maslahi ya baadhi ya nchi za Ulaya hususan Ubelgiji, mkoloni wa zamani wa Burundi.
Warundi wakiandamana na kumuunga mkono Rais Pierre Nkurunziza
Kadhalika waandamanaji wamekosoa msimamo wa António Guterres na kuutaja kuwa unaoingilia masuala ya ndani ya Burundi. Hivi karibuni António Guterres, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa alitoa taarifa mbele ya wajumbe 15 wa Baraza la Usalama la umoja huo akikosoa sisitizo la viongozi wa Burundi kwa ajili ya kuifanyia marekebisho katiba ya nchi hiyo bila kuzingatia maoni ya wapinzani. Katika ripoti hiyo Guterres aliashiria kwamba, juhudi za serikali ya Bujumbura kwa ajili ya kuifanyia marekebisho katiba, zitapelekea kuchochea mzozo kati yake na wapinzani. Ikiwa kura ya maoni itafanyika na kufanyiwa marekebisho ya katiba, basi Rais Pierre Nkurunziza atakuwa na uwezekano wa kusalia zaidi madarakani hadi mwaka 2030.
Rais Pierre Nkurunziza wa Burundi
Hii ni katika hali ambayo Jumatano iliyopita kulianza zoezi la uorodheshaji majina ya wapiga kura katika daftari la kudumu la wapiga kura kwa ajili ya kuwawezesha kushiriki katika kura ya maoni. Mgogoro wa kisiasa nchini Burundi ulianza mwezi April mwaka 2015 baada ya Rais Nkurunziza kutangaza azma yake ya kugombea katika uchaguzi wa rais uliopita, ambapo wapinzani waliitaja hatua hiyo kuwa ni kukiuka katiba huku kwa upande wake serikali ya Bujumbura ikisema kuwa bado rais huyo hajakiuka katiba.

No comments:

Post a Comment