Saturday, February 24, 2018

UN: YAMKINI MAAFISA WA JESHI LA SUDAN KUSINI WAMETENDA JINAI ZA KIVITA

UN: Yamkini maafisa wa jeshi la Sudan Kusini wametenda jinai za kivita
Wakaguzi wa umoja wa Mataifa wanasema zaidi ya maafisa 40 wa Jeshi la Sudan Kusini wanaaminika kutenda jinai za kivita na jinai dhidi ya binadamu.
Wakaguzi hao wa Tume ya Umoja wa Mataifa ya Haki za Binadamu nchini Sudan Kusini wamesema msingi wa uchunguzi wao ni mahojiano waliyofanya na mamia ya mashuhuda, picha za satalaiti na nyaraka 60,000 tokea vita vianze nchini humo mwaka 2013.
Ripoti hiyo ambayo ilichapishwa Ijumaa inasema maafisa wa ngazi za juu jeshini wamehusika na hujuma za makusudi dhidi ya raia. Kati ya wanoatuhumiwa ni maluteni jenerali wanane na magavana wa majimbo matatu.
Hii ni mara ya kwanza kwa ripoti za Umoja wa Mataifa kuhusu Sudan Kusini kuwataja wahusika wa jinai kinyume na miaka ya nyuma ambapo ripoti hizo zilikuwa zikitaja tu jinai zilizotendwa.
Msemaji wa serikali ya Sudan Kusini Mawien Makol amesema serikali ya nchi hiyo iko tayari kumshtaki yeyote aliyehusika na jinai.
Hayo yanajiri wakati ambao Rais Salva Kiir wa Sudan Kusini ametamka bayana kwamba Marekani ndiyo ambayo inasababisha ukosefu wa amani ndani ya nchi yake changa zaidi barani Afrika.
Salva Kiir (kushoto) na Riek Machar
Rais Kiir aliyasema hayo Ijumaa katika mkutano wa viongozi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) mjini Kampala Uganda.
Vita vya ndani nchini humo vilivyoanza Disemba 2013 vimesababisha mauaji ya maelfu ya watu na kulazimisha mamilioni ya wengine kuwa wakimbizi. Nchi hiyo, ambayo ilijitenga na Sudan mwaka 2011, ilitumbukia katika vita vya ndani baada ya Rais Salva Kiir kutoka kabila la Dinka kumtuhumu makamu wake wa zamani, Riek Machar wa kabila la Nuer kwamba alihusika na jaribio la kupindua serikali yake.

No comments:

Post a Comment