Wednesday, February 7, 2018

DOMOKAYA NA MAKELELE YA TRUMP HAYAWEZI KUBADILISHA MAKUBALIANO YA NYUKLIA YA JCPOA

Domokaya na makelele ya Trump hayawezi kubadilisha makubaliano ya nyuklia ya JCPOA
Rais Hassan Rouhani wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amebainisha misimamo ya Tehran kuhusiana na matukio ya kieneo na kimataifa katika mkutano wake na waandishi wa habari wa ndani na wa nje na kusema kuhusiana na makubaliano ya nyuklia ya JCPOA kwamba, katu hakutoongezwa au kupunguzwa chochote katika makubaliano hayo.
Akijubu swali kwamba, Rais Donald Trump amekuwa akisisitiza kuwa, kama makubaliano ya nyuklia ya JCPOA hayatafanyiwa marekebisho, Marekani itaanza tena kuiwekea vikwazo Iran na kwamba, Washington itajitoa katika makubaliano hayo, je katika mazingira haya Ira itachukua uamuzi gani? Rais Rouhani amesema kuwa, Iran haitakuwa ya kwanza kukiuka makubaliano ya nyuklia na hakuna kitakachoongezwa au kupunguzwa katika makubaliano hayo.
Rais Rouhani amesisitiza kwamba, Iran itaendelea kubakia na kufungamana na makubaliano ya nyuklia madhali kuna maslahi na manufaa na kwamba, uamuzi wa Marekani wa kubakia au kujitoa katika makubaliano hautakuwa na taathira yoyote kwa uamuzi wa Jamhuri ya Kiislamu. Kuhusiana na kung'ang'ania Marekani kufanyika mazungumzo mapya kuhusiana na baadhi ya mambo katika makubaliano ya nyuklia na kudhibitiwa mpango wa makombora wa Iran, Rais Hassan Rouhani amesisitiza kwamba, Iran haifuatilii suala la kuwa na silaha za maangamizi ya umati na haribifu kama inavyofanya Marekani na baadhi ya nchi, lakini kuhusiana na silaha za kawaida, Jamhuri ya Kiislamu ya Iran itatengeneza na kumiliki silaha hizo kwa kadiri ya mahitahi ya kiulinzi na kujihami na kwamba, haitafanya mazunguumzo na yeyote kuhusiana na suala hilo.
Rais Hassan Rouhani wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran
Januari 12 mwaka huu, Rais wa Marekani aliongeza kwa mara ya tatu muda wa kusimamishwa vikwazo dhidi ya Iran lakini akatangaza masharti ya kubakia nchi yake katika makubaliano ya nyuklia kama vile kubadilishwa baadhi ya vipengee vya makubaliano hayo, kuruhusu kukaguliwa vituo vya kijeshi vya Iran na kudhoofishwa mpango wa makombora wa Tehran na akasema pia kwamba, endapo Kongresi na Ulaya hazitatekeleza masharti hayo, wakati ujao hataongeza muda wa kusimamishwa vikwazo dhidi ya Iran na nchi yake itajitoa katika makubaliano ya nyuklia ya JCPOA.
Tangu wakati wa kampeni za uchaguzi wa Rais nchini Marekani Donald Trump alitangaza bayana chuki na uadui wake dhidi ya makubaliano ya JCPOA na akasisitiza kwamba, kama atachaguliwa kuwa Rais wa nchi hiyo atayachana makubaliano hayo. Katika radiamali yake kwa msimamo huo wa Trump, Iran ilitoa onyo kali na kusisitiza kwamba, endapo Trump atayachana makubaliano hayo basi Iran itayachoma moto. Msimamo thabiti na imara wa Iran mbele ya serikali ya sasa ya Marekani umemchanganya Trump na washauri wake na hii leo licha ya kupita mwaka mmoja tangu Trump ashike hatamu za uongozi wa White hajaweza kuleta mabadiliko katika makubaliano hayo ya nyuklia.
Bendera ya nchi za kundi la 5+1 zilizofikia makubaliano ya nyuklia na Iran
Juhudi zote za Trump ni kuhakikisha kwamba, kupitia makubaliano ya JCPOA na uropokaji wake aweze kuleta mabadiliko katika siasa za kigeni za Jamhuri ya Kiislamu ya Iran katika Mashariki ya Kati ambapo wenzo huu wa Trump hauwezi kusaidia chochote na wala hauwezi kurejesha nyuma hali ya hivi sasa. Iran ni dola lenye nguvu katika Mashariki ya Kati na imekuwa na taathira katika mahesabu ya eneo na bila shaka makelele kuhusu JCPOA na njama za kutishia uwezo wa makombora  ya Iran ni mambo ambayo kwa hakika hayawezi kumfanya Trump na waungaji mkono wake kama Saudia na Israel kufikia malengo yao.
Nafasi ya Jamhuri ya Kiislamu katika eneo ni nafasi ambayo haiwezi kuathiriwa na mambo yasiyo na maana ya lobi za Wazayuni au domokaya na makelele ya Trump. Nguvu ya Iran katika Mashariki ya Kati chimbuko lake ni uungaji mkono wa wananchi na kutegemea mamlaka yake ya kujitawala na nguvu hii imekuwa na taathira pia kwa eneo hili.

No comments:

Post a Comment