Monday, April 2, 2018

JESHI LA YEMEN LASHAMBULIA KITUO CHA JESHI LA SAUDIA ENEO LA JIZAN

Jeshi la Yemen lashambulia kituo cha Jeshi la Saudia eneo la Jizan
Jeshi la Yemen likishirikiana na wapiganaji wa Harakati ya Ansarullah wamevurumisha kombora la balisitiki ndani ya ardhi ya Saudi Arabia na kulenga kituo cha kijeshi katika eneo la Jizan.
Taarifa zinasema kombora ambalo limetumika katika oparesheni hiyo ni Qaher M-2 ambalo limetengenezwa ndani ya Yemen. Shirika la Habari la Yemen, Saba, limesema kombora hilo limesababisha hasara kubwa katika kituo hicho cha jeshi la Saudia. 
Jumamosi pia Kitengo cha Makombora cha Harakati ya Ansarullah ya Yemen kilitangaza kuwa kimevurumisha kwa mafanikio kombora la balistiki ambalo limelenga kituo cha Jeshi la Saudia katika mkoa wa Najran kusini mwa ufalme huo.
Halikadhalika Ijumaa Harakati ya Ansarullah ilitangaza kuwa ililenga kwa mafanikio kituo cha mafuta cha kampuni ya Aramco ya Saudia katika mkoa wa Jizan. Kombora lililotumika katika iparesheni hiyo pia nia Badr-1. Aidha Jumatatu liyopita wapiganaji wa Ansarullah wakishirikiana na Jeshi la Yemen walishambulia kwa makombora ya balistiki uwanja wa ndege wa kimataifa wa Mfalme Khalid katika mji wa Riyadh mji mkuu wa Saudia, uwanja wa ndege  wa Abha huko Asir na uwanja wa ndege wa Jizan unaopatikana kusini mwa Saudi Arabia. 
Watoto ni waathirika wakuu wa hujuma za Saudia dhidi ya Yemen
Mashambulizi hayo yote ni katika oparesheni za kulipiza kisasi jinai za Saudia dhidi ya raia wa Yemen. Ikumbukwe kuwa Saudia ilianzisha hujuma yake dhidi ya Yemen mnamo Machi mwaka 2015 kwa lengo la kuirejesha madarakani serikali kibaraka ya Abdu Rabuh Mansour Hadi aliyejiuzulu urais na kukimbilia mji mkuu wa Saudia, Riyadh. 
Raia zaidi ya elfu 14  wa Yemen wameuawa, hasa wanawake na watoto, na maelfu ya wengine kujeruhiwa katika uvamizi huo wa kijeshi. Aidha watu karibu milioni moja wameambukizwa ugonjwa wa kipindupindu kote nchini Yemen huku wengine karibu 3,000 wakifariki dunia tokea mwezi Aprili mwaka jana. Mamilioni ya Wayemen pia wamepoteza makazi yao kutokana na hujuma hizo za Saudia.

No comments:

Post a Comment